MAWASILIANO YA BLOG

KWA MAONI NA USHAURI WASILIANA NA OFISI YA HABARI NA MAWASILIANO KWA SIMU NAMBA 0764 143 977 AU E-MAIL: habarigeita@gmail.com

Thursday 9 January 2014


Mkuu wa Mkoa wa Geita Mh. Magalula Said Magalula akifafanua kuhusu utekelezaji wa miradi ya barabara Mkoa wa Geita

MKUU WA MKOA APONGEZA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA BARABARA MKOA WA GEITA
Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Magalula Saidi Magalula amewapongeza viongozi na watu mbalimbali wote waliohusika kwa namna yeyote ile katika usimamizi wa utekelezaji wa miradi yote ya barabara inayotekelezwa ndani ya Mkoa wa Geita.

Mhe. Magalula aliyasema hayo katika kikao maalum cha bodi ya ushauri ya barabara ya Mkoa (Road Board) kilichofanyika Mjini Geita katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri ya Wilaya ya Geita na kuwashirikisha viongozi mbalimbali wa Wilaya,viongozi wa vyama vya siasa na wataalam wa ujenzi wa barabara ambapo walielezwa kwamba Mkoa umepata mafanikio katika utekelezaji wa miradi midogo na mikubwa ya barabara ambayo inaendelea kutekelezwa kwa kiwango cha lami.

Katika kikao hicho Mhe.Mkuu wa Mkoa alizitaka mamlaka za serikali za mitaa pamoja na Tanroads Mkoa wa Geita ziendelee kuhakikisha kwamba shughuli za ujenzi na ukarabati wa barabara zinatolewa kwa wakandarasi wenye vigezo vya uzoefu, uwezo, wataalam na mitambo ya uhakika na pia kufuatilia na kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi hiyo ili kufikia kiwango sahihi na thamani ya fedha ionekane katika miradi husika.

Katika hatua nyingine Mhe. Magalula alizitaka Halmashauri za Wilaya kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu kutovamia hifadhi za barabara na pia kuweka mipaka ya barabara ili kuepusha uharibifu wa barabara. Aidha, alitumia nafasi hiyo kutoa rai kwa wananchi wenye tabia ya wizi wa alama za barabara na kupitisha mifugo katikati ya barabara  na kuacha  mara moja tabia hizo kwani zinasababisha hasara kubwa kwa serikali na  kuziagiza kamati za ulinzi na usalama,ulinzi shirikishi kuweka utaratibu mzuri wa kulinda na kutunza barabara.

Mkoa wa Geita una mtandao wa barabara zenye Kilometa 6,650.75 huku barabara za kiwango cha lami zikiwa ni kilometa 485, changarawe ni kilometa 3,381.05 na barabara za udongo ni kilometa 2,784.70.

Miradi inayotekelezwa kwa kiwango cha lami ni pamoja na ujenzi wa barabara ya “Round about” - Benki ya CRDB - Hospitali ya Wilaya - Benki ya NMB na kuunga barabara kuu ( KM 1) kwa usimamizi wa Tanroads kwa gharama ya Tshs 450 milioni imekamilika kwa asilimia 98.Ujenzi wa barabara ya Nyankumbu-Nyanghwale (km 91) unaendelea kujengwa kwa KM 2 kutoka Nyankumbu hadi Mkolani ujenzi umefikia asilimia 60 na itagharimu kiasi cha million 750 mpaka kukamilisha kilometa 2 za lami ujenzi huo unasimamiwa  na Tanroads. Aidha kuna ujenzi unaoendelea wa barabara ya CRDB- Boman i- Magereza (km1) kwa kiwango cha lami  ambao umefikia asilimia 24 ambao utagharimu Tshs 438 milioni.
Miradi mikubwa ya ujenzi wa barabara inayotekelezwa na serikali na kusimamiwa na Tanroads katika Mkoa wa Geita ni pamoja na Bwanga- Biharamulo (KM 67) kwa gharama ya Tshs 55 bilioni na Bwanga –Uyovu (KM 45) kwa gharama ya Tshs 43.3 bilioni miradi hii yote imefikia asilimia nzuri na iliwekewa jiwe la msingi na Mhe. Rais wakati wa ziara yake Mkoani  Geita.


Na. Magesa Jumapili (Geita)