MAWASILIANO YA BLOG

KWA MAONI NA USHAURI WASILIANA NA OFISI YA HABARI NA MAWASILIANO KWA SIMU NAMBA 0764 143 977 AU E-MAIL: habarigeita@gmail.com

Monday 3 March 2014

MKUU WA MKOA ATEMBELEA WILAYA YA NYANG’HWALE

 

Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Magalula Saidi amefanya ziara  ya kikazi ya siku nne (4) wilaya ya Nyang’hwale Mkoani Geita.


Akiwa katika ziara hiyo Mhe. Mkuu wa wa Mkoa alikagua shughuli mbalimbali kubwa zaidi ikiwa ni ukaguzi wa masuala ya elimu hasa suala la kuwapeleka wanafunzi waliofaulu kuendelea na kidato cha kwanza shuleni katika wilaya hiyo ambapo alizitembelea shule mbalimbali za sekondari  ikiwa ni pamoja Busolwa, Nyijundu, Kafita, Mwingiro,Nyang’hwale na Bukwimba Sekondari.

Aidha katika ziara hiyo Mhe. Mkuu wa Mkoa alizitembelea shule za msingi mbalimbali kwa lengo la kukagua suala la utengenezaji wa madawati na uandikishwaji wa wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza ambapo aliwataka wazazi wote kuwapeleka watoto wao shuleni hivyo hivyo walivyo wakati taratibu za kutimiza mahitaji yao zikifanyika wanafunzi wakiwa shuleni.

Katika hatua nyingine Mhe. Magalula Saidi aliwataka viongozi wa kata na vijiji kuwachukulia hatua kali za kisheria wazazi wote ambao hawajawapeleka watoto wao shule ikiwa ni pamoja na kuwafikisha mahakamani .

Sambamba na hilo Mhe. Mkuu wa Mkoa alifanya mikutano  ya hadhara katika maeneo yote aliyopita wakati wa ziara yake ambapo alikemea vitendo vya kujichukulia sheria mkononi na kuwauwa watu wasiokuwa na hatia kwa kisingizio cha imani za kishirikina na hasira kali.

Ziara hiyo imesaidia sana kuamsha ari ya wananchi kupenda kuwapeleka watoto shule na pia kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi.

Na: Magesa Jumapili