MAWASILIANO YA BLOG

KWA MAONI NA USHAURI WASILIANA NA OFISI YA HABARI NA MAWASILIANO KWA SIMU NAMBA 0764 143 977 AU E-MAIL: habarigeita@gmail.com

Wednesday 19 March 2014

WAKURUGENZI WA HALMASHAURI ZA MKOA WA GEITA WATAKIWA KUWEKA UTARATIBU MZURI WA KUVIPELEKA VIKUNDI VYA WAFUGAJI NYUKI KWENDA KUJIFUNZA NAMNA YA UFUGAJI NYUKI BORA WILAYANI BUKOMBE

Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Magalula Saidi akitundika mzinga wakati wa siku ya maadhimisho ya siku ya kutundika mizinga ambayo katika Mkoa wa Geita maadhimisho hayo yamefanyika katika kijiji cha Ikina kata ya Bukoli Wilaya ya Geita.

WAKURUGENZI GEITA WATAKIWA KUWEKA UTARATIBU MZURI KWA VIKUNDI KWENDA KUJIFUNZA UFUGAJI NYUKI WILAYA YA BUKOMBE:

Wakurugenzi  wa Halmashauri za wilaya Mkoani Geita wametakiwa kuweka utaratibu mzuri wa vikundi vya wafuga nyuki kwenda kujifunza namna bora ya ufugaji nyuki katika wilaya ya Bukombe ambayo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika zao la nyuki.


Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya utundikaji wa mizinga ya nyuki ambayo imefanyika kimkoa katika kijiji cha Ikina wilaya ya Geita Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe.Magalula Saidi ametoa wito kwa wakurugenzi wote wa halmashauri za wilaya Mkoani hapa kuhakikisha kuwa wanaweka utaratibu mzuri kwa vikundi vyote vya wafugaji wa nyuki kwenda wilaya ya Bukombe  ili wakaone namna wafugaji wa nyuki wa huko walivyo piga hatua katika shughuli hiyo ili nao wanufaike.

“Natoa wito kwa wakurugenzi wote kuweka utaratibu mzuri wa kuwapeleka wafugaji wa nyuki wilaya ya Bukombe ili wakaone namna wenzao wanavyozalisha na kujipatia kipato na maendeleo kwa kutumia fursa ya ufugaji nyuki kwani wilaya hiyo imewahi kutoa mshindi wa kitaifa katika uzalishaji wa asali na ufugaji nyuki”.

Katika maadhimisho hayo Mkuu wa Mkoa alikabidhi mizinga 50 ya nyuki kwa kikundi cha wafugaji nyuki cha Ikina ambapo alitumia nafasi hiyo kuwapongeza wanakijiji hao kwa jitihada hizo na kuwataka kuendelea na moyo huo katika kujiletea maendeleo kupitia mradi wa nyuki. Aidha Mhe. Mkuu wa Mkoa alimpongeza mzee Faustine Ntaliyo ambaye alijitolea shamba lake la msitu wa asili lenye hekta 25 litumike katika shughuli za kikundi hicho za ufugaji wa nyuki.

Halikadhalika Mhe. Mkuu wa Mkoa aliwapongeza wakala wa huduma za misitu (TFS) kwa jitihada zao za kuwasaidia wafugaji wa nyuki mizinga na kuzitaka taasisi zingine za umma na binafsi kutoa misaada ya mizinga kwa vikundi mbalimbali vya wafugaji wa nyuki ndani ya Mkoa wa Geita ili navyo vinufaike na miradi ya  nyuki.Aliwataka wananchi wote wa Mkoa wa Geita kuwekeza katika ufugaji wa nyuki kwani hiyo ni  fursa ya kujiletea kipato na maendeleo katika kaya.

Katika maadhimisho hayo Mhe.Magalula aliwataka maafisa biashara kuhakikisha kuwa wanatafuta masoko ya uhakika ya asali na lakini pia maafisa nyuki wahakikishe wanatoa ushauri wa kitaalam kwa wafugaji nyuki ili wazalishe kwa wingi na ubora.

Halmashauri ya wilaya ya Geita imeahidi kuwa kukipatia kikundi hicho mabati ishirini 20 ambayo yatasaidia kufunika mizinga ili kuiepusha kulowana kwa maji ya mvua kitendo ambacho kitasaidia ubora wa asali pamoja na kutokuhama kwa nyuki.Hatahivyo kikundi hicho kiliishukuru serikali kupitia wakala wa misitu kwa kuwapatia mizinga hiyo 50 ya kisasa yenye mifuniko iliyozibwa kwa juu na kuahidi kuitunza ili iweze kuwapatia faida.

Mkoa wa Geita ni mmoja wa mikoa ambao unazalisha asali yenye ubora wa hali ya juu hasa wilaya ya Bukombe ambayo iliwahi kutoa mshindi wa kitaifa katika ufugaji wa nyuki.

Na: Magesa Jumapili (Geita)